Jumatano, 12 Agosti 2015

Habari Mpya Kutoka MUHIMBILI Ambako Freeman Mbowe Amelazwa Baada ya Kuugua Ghafla


Hali ya mwenyekiti wa CHADEMA taifa na mbunge wa jimbo la Hai anayemaliza muda wake, mh Freeman Aikae Mbowe, imeendelea kuimarika.
Akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi uliopita katika Hospitali ya taifa ya Muhimbili, anakopatiwa matibabu, mh Mbowe, amesema anaendelea vizuri na kwamba bado anaendelea kupumzika hospitalini hapo, kama alivyopangiwa na madaktari wanaoangalia hali yake.
”Hali yangu imeendelea kuimarika na kilichonipata jana kwa mujibu wa uchunguzi wa madaktari ni uchovu wa muda mrefu, uliobainishwa kutokana na shughuli za muda mrefu bila kupumzika katika shughuli zangu za kisiasa” amesema Mbowe.
Mh Mbowe ameongeza kwamba, madaktari wamemtaka kuendelea kuwa chini ya uangalizi wao mpaka hapo watakapo mruhusu kuendelea na shughuli zake za kwawaida.
Mmoja kati ya madaktari wanaoangalia afya ya mh Mbowe, Dr Tulizo Sanga(daktari bingwa wa magonjwa ya moyo) ,amewaambia waandishi wa habari hospitalini hapo kwamba, mh Mbowe alipokelewa jana akitokea Hospitali ya Doctors Mall ya Kinondoni,jijini Dar Es Salaam, kwa ajili ya uangalizi na uchunguzi zaidi kutokana na kuugua ghafla wakati akiwa katika msafara wa mgombea urais wa CHADEMA, Edward Lowassa.
Mh Mbowe amelazwa katika hospitali ya Muhimbili, kitengo cha moyo, baada ya kuugua ghafla jana na kukimbizwa hospitalini hapo.
 
Nae James Mbatia mwenyekiti wa NCCR Mageuzi, ambaye pia ni mwenyekiti mwenza wa UKAWA, amefika hospitalini hapo kumjulia hali mh Mbowe, na amesema pamoja na hali ya kuumwa ya mh Mbowe, wao bado wanaendelea kufanya kazi na kwamba ratiba mbalimbali za vikao vya UKAWA ziko palepale, na amewaomba watanzania kuwa watulivu na kuendelea kumuombea mh Mbowe, apone haraka.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni